WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema mji wa Dodoma ni lazima upangwe ili uwe tofauti na miji mingine nchini.
Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo jana wakati akizungumza na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Moladi Tanzania, Abeid Abdallah ambaye alifika ofisini kwake Magogoni, jijini Dar es Salaam na kuelezea nia yake ya kutaka kuwekeza mjini Dodoma.
Amesema serikali haitaki kurudia makosa yaliyofanyika kwenye miji mingine.
“Katika kuupanga ule mji, ni lazima mji upangwe kama ambavyo miji mingine mikuu inapangwa. Kila eneo kutakuwa na nyumba za aina fulani. Hatuwezi kuachia watu wajenge popote na wanavyotaka, mji unakuwa haupangiki. Na hilo ndilo kosa lililofanyika kwenye miji mingine mikubwa ambayo tunayo kwa sasa,” alisema Majaliwa katika taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu.
Alisema Kamati ya Kitaifa ya Maandalizi ya kuhamia Dodoma imepewa jukumu la kupitia upya Master Plan ya mji wa Dodoma na kuainisha maeneo ambako nyumba za aina mbalimbali zitajengwa.
Akizungumzia kuhusu ujenzi kwenye maeneo ambayo tayari wananchi wanaishi, Waziri Mkuu amesema serikali itaweka utaratibu ili kuwe na mikataba baina ya mwekezaji na mwananchi anayemiliki eneo husika ili asinyimwe haki ya kumiliki eneo lake.
Abdalla alimweleza Waziri Mkuu kwamba wako tayari kushirikiana na serikali katika kazi ya serikali kuhamia Dodoma kwa lengo wa kuwasaidia wananchi wa kipato cha chini kupata makazi bora na ya kudumu.
Hakuna maoni :
Chapisha Maoni