TAARIFA HUKUJUZA MENGI YA ULIMWENGUNI

Jumatatu, 4 Aprili 2016

KILA MMOJA WETU ANAHAKI YAKE YA KUPATIWA KILE KILICHOBORA ZAIDI KWAKE TUSITENGANE

Hakuna maoni
SERIKALI imesema inafanya juhudi za makusudi kuhakikisha kuwa watoto wenye mahitaji
maalumu wanapata elimu sawa na wengine, ambapo mkazo wa sasa ni kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji.
Hayo yalibainishwa mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Stella Manyanya, wakati wa kuadhimisha Siku ya watu wenye usonji duniani, kwa niaba ya Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, yalíyofanyika katika Shule ya Msingi ya Al-Muntazir Upanga.
“Kwa sasa tunaendelea kuandaa walimu wenye ujuzi na maarifa ya elimu maalumu, kuboresha miundombinu na huduma za kitabibu kwa ajili ya kuwahudumia watoto wenye usonji na mahitaji maalumu kwa ujumla,” alisema.
Aliitaka jamii kuwachukulia watoto wenye mahitaji maalumu kama sehemu ya jamii na kuwashirikisha katika nyanja zote za maendeleo. Pia aliwataka wazazi, walezi na jamii kuwapa kipaumbele bila kujali tofauti za kimaumbile na kuhakikisha wanapata fursa ya elimu.
Alisema usonji ni upungufu wa kibayolojia anaompata mtoto anapokuwa tumboni mwa mama yake na dalili zake huonekana kuanzia umri wa miaka mitatu na kuendelea. Alisema kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), wamepima kila watoto 160, wanaozaliwa duniani mmoja anakuwa na usonji.
“Watoto hawa wakipata maarifa na stadi za kuwawezesha kujumuika na kujitegemea watapunguza hali ya utegemezi na kutoa fursa kwa wazazi na wao wenyewe katika kujitafutia maendeleo,” alisema.
Alisema katika jamii ya kitanzania uelewa wa jamii bado ni mdogo na huduma inayotolewa kwa watu wenye usonji si ya kuridhisha ambapo wanakuwa na fikra potofu na imani za kishirikina na kwamba ni miongoni yanayotajwa kukwamisha juhudi za kitabibu kwa watoto hao.
Aidha, alisema vyombo vya habari vina mchango mkubwa katika kuelimisha na kuhamasisha wazazi, walezi na jamii kwa ujumla ili isiwafiche au kuwanyanyapaa watoto wenye ulemavu, badala yake watumie fursa zilizopo ili kuhakikisha kuwa watoto wanapata haki za msingi ikiwemo elimu.
Alisema serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi na wadau wa elimu imekuwa ikipanua fursa za upatikanaji wa elimu kwa watoto wenye mahitaji maalum kwa kuandaa walimu, kuboresha miundombinu kwa wanafunzi wenye mahitaji maalumu katika elimu.
Alishukuru uongozi wa Taasisi ya Khoja Shia Itha Asheri Jamaat (KISJ) kwani imekuwa mstari wa mbele katika kuwahudumia watoto wenye usonji na mahitaji mengine maalumu kwa kuwapa elimu na huduma nyingine za jamii.

Hakuna maoni :

Chapisha Maoni